Tanzania Consulate General in Guangzhou

Tanzania Consulate General in Guangzhou

Share

Tanzania-Guangzhou cooperation. Consulate General of Tanzania in Guangzhou, China!

01/05/2026

Tunasherehekea juhudi na mafanikio ya wafanyakazi wote duniani. Kila mchango ni muhimu, na leo tunathamini kazi ngumu na kujitolea kwa kila mmoja. Tujivunie na tushirikiane katika kujenga jamii yenye mafanikio na ustawi. Heri ya Siku ya Wafanyakazi!

Photos from Tanzania Consulate General in Guangzhou's post 25/04/2026

Ofisi ya Konseli Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania jijini Guangzhou, kwa kushirikiana na Jumuiya ya Watanzania waishio Guangzhou kupitia kongamano la Tanzania Bussiness Connect 2026 wamefanikiwa kuwakutanisha wadau mbalimbali wa biashara wakiwemo wafanyabiashara kutoka Tanzania na China, taasisi za fedha za Tanzania, jumuiya za wafanyabiashara, wanafunzi pamoja na makampuni ya usafirishaji mizigo kati ya Tanzania na China.

Kongamano hilo limejadili masuala mbalimbali yenye kulenga kukuza biashara, hususan katika kipindi hiki cha maonyesho ya kimataifa ya yanayoendelea. Lengo kuu lilikuwa ni kujenga mtandao (networking), kuimarisha ushirikiano wa kibiashara, kuunganisha wazalishaji na wanunuzi, pamoja na kujadili changamoto zinazoweza kujitokeza katika biashara za kimataifa, hasa zile zinazohusisha uvukaji wa mipaka.

Akizungumza katika kongamano hilo, Konseli Mkuu Ndg aliwahimiza Watanzania, hususan wafanyabiashara, kutumia vyema fursa za kitakwimu zinaoonesha kuwa China ni mshirika mkubwa wa kibiashara wa bara la Afrika. Aidha, alieleza maeneo muhimu ambayo Tanzania inaweza kuyatumia kunufaika zaidi na ushirikiano huo, ikiwa ni pamoja na eneo lake la kijiografia, hali ya amani na utulivu, uwepo wa Serikali yenye Uongozi thabiti, mifumo rafiki kwa wawekezaji, pamoja na wingi wa rasilimali zilizopo Tanzania.

Kwa ujumla, kongamano hilo limekuwa na mafanikio makubwa na limeonyesha mwitikio chanya kutoka kwa washiriki, likilinganishwa na tukio k**a hilo lililofanyika mwaka jana. Tanzania Business Connect 2026 Limeendelea kuwa jukwaa muhimu la kukuza mahusiano ya kibiashara kati ya Tanzania na China.

Photos from Tanzania Consulate General in Guangzhou's post 24/04/2026

Kwa ufadhili wa benki za Azania, na CRDB, na kwa uratibu wa Chemba ya Wanawake Wafanyabiashara Tanzania (TWCC), kundi la wafanyabiashara na Wajasiliamali kutoka Tanzania limefanikiwa kufanya ziara jijini nchini China kwa lengo la kutafuta fursa za biashara na kupata mafunzo ya kuboresha ufanisi wao.

Katika ziara hiyo, washiriki walitembelea masoko mbalimbali ya kimataifa, kukutana na wazalishaji na wanunuzi, pamoja na kushiriki katika maonyesho makubwa ya biashara ya . Kupitia ziara hiyo, washiriki wameweza kujifunza mbinu mpya za biashara, kuongeza uelewa wa soko la kimataifa, na kujenga mtandao muhimu wa kibiashara.

Katika siku ya mwisho ya ziara, washiriki walipata fursa ya kukutana na Konseli Mkuu Ndg Khatibu Makenga kwa ajili ya tathmini ya mafanikio ya ziara hiyo na kupata miongozo na mwelekeo wa kimkakati kwa ziara nyingine k**a hizo.

Miongoni mwa mambo muhimu yaliyosisitizwa ni pamoja na usimamizi mzuri wa mitaji, uelewa wa misimu ya biashara, na umuhimu wa kupanua masoko kwa kutembelea maeneo mbalimbali nchini China tofauti ya yale yaliyozoeleka.

Washiriki wameeleza kuridhishwa na ziara hiyo na kuahidi kutumia maarifa waliopata kuboresha biashara zao na kuchangia ukuaji wa uchumi. Ziara imehitimishwa rasmi, na washiriki wanarejea nyumbani wakiwa na ari mpya na dira ya mafanikio.

Photos from Tanzania Consulate General in Guangzhou's post 22/04/2026

Maafisa wa benki ya NBC, Bw. M***a Mwinyidaha kutoka Idara ya Biashara, Wateja Wadogo na wa Kati, Bi. Prisca Ngonyani kutoka Idara ya Diaspora, na Bw. Fakihi Mwanga kutoka Idara ya Mikopo – Wateja Wadogo na wa Kati, walifanya ziara rasmi katika Ofisi ya Konseli Kuu na kukutana na Konseli Mkuu, Ndg. Khatibu Makenga. Lengo kuu la ziara hii lilikuwa kujitambulisha na kuwasilisha mikakati ya benki hiyo katika kuboresha huduma za kifedha na kushirikiana na Watanzania waishio nje ya nchi, hususan wale wanaoishi nchini China.

Katika mazungumzo hayo, maafisa wa NBC walisisitiza dhamira ya benki hiyo katika kuboresha huduma za kifedha kwa Watanzania waishio nje, kupitia uwezeshaji wa uwekezaji na kurahisisha miamala ya kimataifa. Walieleza pia mikakati ya benki katika kutoa huduma bora kwa wateja wadogo na wa kati, ikiwa ni pamoja na huduma za mikopo, kuwezesha biashara ndogo na kati, na kuhamasisha Watanzania kuwekeza katika fursa mbalimbali za kifedha zilizopo.

Aidha, NBC ilibainisha kuwa benki hiyo ni miongoni mwa wadhamini wa kongamano la pili la biashara linalotajwa k**a Tanzania Business Connect 2026, litakalofanyika tarehe 24 Aprili 2026. Kongamano hili linashirikisha ushirikiano kati ya Ofisi ya Konseli Kuu ya Tanzania na Jumuiya ya Watanzania waishio Guangdong (DITAG), ambapo lengo kuu ni kuunganisha fursa za biashara na uwekezaji kati ya Watanzania na wazalishaji wa China. Kongamano hili pia linajadili mbinu bora za kushirikiana na wafanyabiashara wa kimataifa, na jinsi ya kukabiliana na changamoto za biashara ambazo Watanzania wanakutana nazo kutokana na uzoefu mdogo katika masuala ya biashara ya kimataifa.

NBC imeonyesha kujitolea kwa dhati katika kuboresha huduma zake kwa jamii ya Watanzania waishio nje, ikiwa ni sehemu ya mikakati yake ya kupanua huduma na kuleta manufaa kwa pande zote mbili, Tanzania na China. Benki hiyo inaendelea kuweka mikakati ya kuhakikisha kuwa huduma zinazotolewa zinakidhi mahitaji ya wateja, hasa katika kipindi hiki cha mabadiliko makubwa katika sekta ya biashara na teknolojia.

Kwa kushirikiana na Ofisi ya Konseli Kuu na DITAG, NBC inatarajia kuwa na mchango mkubwa katika kukuza biashara na uwekezaji kwa Watanzania waishio nje ya nchi, na hivyo kuongeza ushirikiano wa kiuchumi kati ya Tanzania na China. Mikakati hii ya benki inatoa matumaini kwa Watanzania wanaoishi China kwa ajili ya kuboresha hali zao za kifedha na kuwawezesha kufikia fursa zaidi za maendeleo.

Photos from Tanzania Consulate General in Guangzhou's post 21/04/2026

Chuo Kikuu cha Lugha za Kigeni cha Guangdong (GDUFS) kimekubali kusaini mkataba wa makubaliano (MoU) na Chama cha Wanawake Wanaomiliki Shule nchini Tanzania (TAWASCO) kufuatia ziara ya ujumbe wa chama hicho katika chuo hicho jijini Guangzhou.

Ziara katika Chuo hicho ilianza kwa mkutano ambao uliitoa fursa ya kujifunza na kubadilishana uzoefu kuhusu namna chuo hicho kinavyoendesha shughuli zake, hususan katika utoaji wa elimu bora na ujenzi wa miundombinu rafiki kwa wanafunzi wote, wakiwemo wenye ulemavu.

Kupitia mkataba huo, TAWASCO inatarajia kunufaika na ushirikiano wa karibu utakaowezesha programu za kubadilishana walimu na wanafunzi, pamoja na kushirikiana katika maendeleo ya taaluma kwa kutumia nyenzo na mifumo ya kisasa ya elimu.

Katika mkutano huo, Konseli Mkuu Ndg Khatibu Makenga alizihimiza taasisi zote mbili kuweka jitihada za dhati kuhakikisha kuwa mkataba huo unasainiwa mapema chini ya usimamizi wa Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia ya Tanzania, na kwamba matokeo ya awali ya ushirikiano huo yaanze kuonekana kabla ya mwezi Desemba 2026.

Photos from Tanzania Consulate General in Guangzhou's post 19/04/2026

Konseli Mkuu, Ndg Khatibu Makenga, amefanya ziara katika ofisi za Makao makuu ya kampuni ya Haid Group, iliyopo katika Wilaya ya Panyu, Jijini Guangzhou kwa lengo la kupokea taarifa ya hatua iliyofikia kampuni hiyo katika uwekezaji wake nchini Tanzania. Kampuni hiyo inashughulika na uzalishaji wa mbegu za mimea na wanyama, chakula cha mifugo, pamoja na shughuli za ufugaji kwa lengo la kuhudumia wazalishaji wengine, wafugaji na watumiaji kwa ujumla.

Kampuni hiyo tayari imefanya ziara nchini Tanzania mara kadhaa kwa lengo la kufanya tafiti za awali ili kutekeleza dhamira ya kuwekeza katika uzalishaji wa chakula cha mifugo, ufugaji wa kuku wa mayai, pamoja na ufugaji wa wanyama. Kampuni hiyo imeeleza hatua zilizofikiwa ili kuiwezesha Serikali kutoa msaada unaohitajika katika hatua zinazofuata.

Kampuni hiyo tayari imepata eneo la kufanya uwekezaji katika mikoa ya Pwani na Mwanza na sasa wamewasilisha rasmi barua ya nia kwa uwekezaji wa miradi hiyo mitatu itakayoanza kutekelezwa baada ya hatua za uwekezaji kupitia TISEZA kukamilika.

Photos from Tanzania Consulate General in Guangzhou's post 16/04/2026

Maonesho ya Kimataifa kuhusu Maendeleo ya Kilimo na Ubidhaishaji (The International Conference on Branded Agriculture Development) yalifanyika katika Mji wa Dongguan, Jimbo la Guangdong, kuanzia tarehe 11 hadi 13 Aprili 2026. Maonesho hayo yalijumuisha wadau wakuu kutoka sekta ya biashara ya kilimo, watunga sera, na wawekezaji kutoka kote duniani, na yalilenga kujadili mikakati ya kujenga chapa (brand) imara za mazao ya kilimo, kuboresha minyororo ya thamani, na kukuza bidhaa bora za kilimo zinazoweza kushindana sokoni.

Kwa upande wa Tanzania, Ofisi ya Konseli Kuu ilishiriki katika mkutano wa ufunguzi wa maonesho hayo, ambapo washiriki walipata fursa muhimu ya kujifunza teknolojia za kisasa za kilimo, mbinu za kutengeneza brand, na ufungashaji wa bidhaa, pamoja na kuimarisha uhusiano wa kibiashara na masoko ya China na kimataifa.

Fursa hii inagusa moja kwa moja wazalishaji, wachakaji, wafungashaji, na wauzaji wa mazao ya kilimo ambayo tayari yamepata soko nchini China, k**a vile kahawa, chai, korosho, mazao ya bahari, na mazao ya bustani. Kupitia kujifunza kuhusu brand zenye nguvu kimataifa, wadau hawa wataweza kubadilisha mitazamo ya biashara na kuleta tija, kuvutia mauzo ya nje, kuvutia uwekezaji, na kuchangia maendeleo endelevu ya sekta ya kilimo nchini Tanzania.

Photos from Tanzania Consulate General in Guangzhou's post 12/04/2026

Konseli Mkuu, Ndg. Khatibu Makenga, amepokea ujumbe wa wanawake 58 kutoka Tanzania ambao ni wanachama wa Chama cha Wanawake Wanaomiliki Shule za Sekondari Tanzania (TAWOSCO), ukiongozwa na Bibi Christa Rweyemamu, Makamu Mwenyekiti wa chama hicho. Ujumbe huu unashiriki katika Maonyesho ya Kimataifa ya Biashara ya Canton , pamoja na kufanya ziara katika miji na maeneo mbalimbali kwa lengo la kujionea na kujifunza kuhusu fursa zinazopatikana katika sekta ya elimu.

Katika ziara hiyo, moja ya maeneo makuu ya kipaumbele kwa ujumbe huu ni matumizi ya teknolojia ya e-learning. Wanachama wengi wameonesha dhamira ya kuboresha na kuibadilisha mifumo ya shule zao ili iendane na maendeleo ya kiteknolojia, ikiwemo kuhuisha mitaala, kuboresha mazingira ya kujifunzia, pamoja na kuinua viwango vya miundombinu na muonekano wa shule zao. Aidha, watapata fursa ya kutembelea shule za sekondari, vyuo vikuu, kushiriki mafunzo kwa vitendo, na kufanya mazungumzo na viongozi wa Idara ya Elimu katika Jimbo la Guangdong.

Ziara hii inatarajiwa kudumu kwa takribani wiki mbili, ambapo washiriki watapata uzoefu mpana, maarifa mapya, pamoja na fursa za kujenga mitandao na ushirikiano wa kimkakati. Matokeo ya ziara hii yanatarajiwa kuchangia kwa kiasi kikubwa katika kuboresha sekta ya elimu nchini Tanzania kupitia ubunifu, teknolojia, na mbinu bora za ufundishaji na uendeshaji wa taasisi za elimu.

Photos from Tanzania Consulate General in Guangzhou's post 09/04/2026

Konseli Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Jiji la Guangzhou, Ndg , ametoa hotuba kwa Kiswahili katika sherehe za tamasha la tatu la tamaduni za nchi za Asia na Afrika lililoandaliwa na Chuo Kikuu cha Guangdong cha Lugha za Kigeni (Guangdong University of Foreign Studies). Katika hotuba yake, Ndg Makenga alisisitiza umuhimu wa lugha k**a sehemu ya utamaduni ambapo huunganisha jamii na kuimarisha ushirikiano kati ya mataifa.

Aidha, alikishukuru chuo hicho kwa kuanzisha Kozi ya Shahada ya Kwanza ya lugha ya Kiswahili Septemba 2025, huku akieleza kuwa hatua hiyo itaongeza uelewa wa utamaduni wa Kiswahili na kuimarisha mahusiano kati ya China na Tanzania katika nyanja za elimu, na mahusiano ya mtu na mtu. Mwisho, aliahidi kuwa Serikali ya Tanzania iko tayari kutoa ushirikiano unaohitajika ili kuimarisha ufundishaji wa lugha ya Kiswahili chuoni hapo.

21/03/2026

Kutoka hapa tunawatakia Eid Mubarak! 🌙✨, siku hii tukufu iwe yenye amani, furaha na baraka tele. Mwenyezi Mungu akubali ibada zenu na awajalie afya njema, mafanikio na upendo usio na kikomo. Eid njema! 🤍

16/03/2026

Nchini hukutana watu kutoka mataifa mbalimbali kwa ajili ya elimu, biashara na utafiti. Watanzania waliopo China hupata nafasi ya kujenga mitandao ya kitaaluma na kibiashara na watu kutoka sehemu tofauti za dunia. Mitandao hii inaweza kuwa muhimu kwa kupata ushirikiano wa miradi, fursa za ajira, au ubadilishanaji wa maarifa unaoweza kusaidia maendeleo ya mtu binafsi na jamii yake.

Want your business to be the top-listed Government Service in Guangzhou?

Click here to claim your Sponsored Listing.

Location

Telephone

Address

International Commerce Center, Unit C, Room 3702, 37th Floor, No. 235 Tianhe North Road, Tianhe District
Guangzhou
510610