08/06/2026
KINONDONI YAIDHINISHA MPANGO MKAKATI WA KUPUNGUZA TAKA ZA PLASTIKI
Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni imeidhinisha Mpango Mkakati wa Kupunguza Taka za Plastiki wa miaka mitano kuanzia mwaka 2026 hadi 2031, ukiwa na lengo la kuimarisha usimamizi wa mazingira na kupunguza athari za taka katika maeneo ya fukwe, mito, mifereji ya maji, barabara na maeneo mengine ya umma.
Kwa mujibu wa mpango huo ambao utatekelezwa na Manispaa ya Kinondoni kwa kushirikiana na Taasisi ya FORUM CC na IUCN unatarajia kufikia asilimia 90 ya ukusanyaji na udhibiti wa taka za plastiki ifikapo mwaka 2029 kupitia kuimarisha mifumo ya ukusanyaji taka, kuongeza uhamasishaji kwa wananchi na kushirikisha wadau mbalimbali katika shughuli za usimamizi wa mazingira.
Akizungumza katika kikao cha kuidhinisha mpango huo, Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Saad Mtambule, amesema Kinondoni imepiga hatua kubwa katika usimamizi wa mazingira na usafi ikilinganishwa na miaka ya nyuma.
Aidha, amesisitiza umuhimu wa kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu athari za taka za plastiki, kuimarisha utekelezaji wa sheria za mazingira na kuongeza ushirikiano wa wadau mbalimbali ili kuhakikisha malengo ya mpango huo yanafikiwa.
.hmwinyi
06/06/2026
Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Saad Mtambule, amesisitiza umuhimu wa upandaji na utunzaji wa miti ili kuunga mkono juhudi za Serikali katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.
Akizungumza Katika katika Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yaliyofanyika jana Juni 5,2026 Kinondoni, Mtambule alisema upandaji wa miti ni muhimu katika kuboresha mazingira na kuhakikisha ustawi wa vizazi vya sasa na vijavyo.
"Tupande miti kwa wingi na tuihudumie ili ikue. Hii ni njia muhimu ya kulinda mazingira yetu na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho," alisema Mtambule.
Pia aliipongeza Manispaa ya Kinondoni, Baraza la Madiwani, wakandarasi wa usafi na wadau mbalimbali kwa mchango wao katika kuimarisha usafi wa mazingira, hatua iliyochangia wilaya hiyo kutokuwa na magonjwa ya mlipuko kwa takribani miaka mitatu.
Aidha, aliwataka wakandarasi wa usafi kuongeza ufanisi katika ukusanyaji na uondoshaji wa taka pamoja na kuwekeza katika vifaa na magari ya kisasa ili kuimarisha huduma za usafi na kukidhi mahitaji ya wilaya inayokua kwa kasi.
05/06/2026
Wadau mbalimbali wa mazingira kutoka Wilaya ya Kinondoni (Sekondari ya Makumbusho, Euro gas Limited, Mtaa wa Mapito , Umoja wa wanawake, suma Jkt na Ngalawa Investment) wametunukiwa tuzo za pongezi kwa mchango wao katika utunzaji na uhifadhi wa mazingira.
Tuzo hizo zimetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Mhe. Edward Mpogolo, kwenye kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yaliyofanyika leo Juni 5, 2026 katika Viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam, ambapo alimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila.
Akizungumza katika maadhimisho hayo, Mhe. Mpogolo amesema, ni muhimu kutumia vifaa vya kisasa vya usafi ili kukabiliana na changamoto za mazingira, kuboresha muonekano wa miji na kuimarisha taswira ya nchi.
Aidha, amesisitiza matumizi ya nishati safi, kuepuka ukataji miti ovyo na kuendelea kuhifadhi mazingira kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo, sambamba na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kupitia utunzaji wa mazingira.
05/06/2026
WANANCHI KATA YA KAWE WAHIMIZWA KUUNGA MKONO JUHUDI ZA UHIFADHI WA MAZINGIRA
Wananchi wa Kata ya Kawe Manispaa ya Kinondoni wamehimizwa kuunga mkono juhudi za Serikali katika kutunza, kuhifadhi na kusafisha mazingira, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya kilele cha Siku ya Mazingira Duniani.
Wito huo umetolewa leo Juni 5, 2026 na Mtendaji wa Kata ya Kawe, Bi. Husna Nondo, wakati wa zoezi la usafi wa mazingira lililofanyika katika ufukwe wa Kawe, kwa kushirikiana na NEMC, Airtel, CAMUSAT na Wananchi wa Kata hiyo kwa lengo la kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa mazingira safi na salama.
Akizungumza wakati wa zoezi hilo, Bi. Husna amesema, Wananchi wanapaswa kuunga mkono juhudi za Serikali na wadau wa mazingira kwa kuzingatia sheria, kanuni na elimu inayotolewa kuhusu utunzaji wa mazingira ili kulinda afya ya jamii, ambayo msingi wake ni mazingira safi na salama.
“Namna pekee ya kulinda mazingira ni kuunga mkono juhudi za Serikali na wadau kwa ajili ya kuhakikisha usalama na ustawi wa mazingira kwa vizazi vya sasa na vijavyo,” alisema Bi. Husna.
Kwa upande wake, Afisa Mazingira kutoka Baraza la Taifa la Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Bw. Gilbat Mboma, ameipongeza kampuni ya Airtel kwa kuendelea kuwa mstari wa mbele katika kampeni za utunzaji wa mazingira kwa kushirikiana na taasisi mbalimbali za Serikali.
Amesema hatua hiyo inaonesha dhamira ya dhati ya sekta binafsi katika kuunga mkono maono ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kuhakikisha mazingira yanatunzwa, kaulimbiu isemayo: “Dira 2050: Tuwajibike Kukijanisha Tanzania,”.
04/06/2026
Kamati ya Fedha na Uongozi ya Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni ikiongozwa na Mstahiki Meya, Mhe. Songoro Mnyonge, leo Juni 4, 2026 imefanya ziara ya kutembelea miradi ya "Zero Waste" katika Shule ya Sekondari Kibasila na Shule ya Msingi Taifa zilizopo Manispaa ya Temeke kwa lengo la kujifunza namna miradi hiyo inavyosimamia taka na kuzigeuza kuwa mbolea.
Ziara hiyo imelenga kupata uzoefu wa mbinu mbalimbali zinazotumika katika usimamizi wa taka kwenye shule hizo ili maarifa na ujuzi huo viweze kutumika katika shule za Manispaa ya Kinondoni, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha usafi wa mazingira na usimamizi endelevu wa taka.
Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mhe. Songoro amesema miradi ya "Zero Waste" ni suluhisho muhimu katika kuimarisha usafi wa mazingira na kuwajengea wanafunzi uelewa pamoja na stadi za utunzaji wa mazingira kupitia matumizi sahihi ya taka zinazozalishwa shuleni, hususan taka zinazo oza.
“Utekelezaji wa mradi huu katika Manispaa ya Kinondoni utaenda kusaidia kwa kiasi kikubwa katika utunzaji wa mazingira ya shule zetu lakini pia uzalishaji wa mbolea inayoweza kutumika katika bustani na shughuli nyingine za kilimo shuleni” amesema Mhe. Songoro.
04/06/2026
Kuelekea kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani tarehe 05 juni, 2026, Manispaa ya Kinondoni imepanda miti zaidi ya 5,000 katika maeneo mbalimbali ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha uhifadhi wa mazingira na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia ya nchi.
Akizungumza wakati wa zoezi hilo leo Juni 4, 2026, Afisa Mazingira wa Manispaa ya Kinondoni, Bw. Anaeli Elibariki, amesema miti ya matunda na vivuli imepandwa katika shule, kando ya barabara na katika Taasisi mbalimbali ili kuendelea kuboresha na kuhifadhi mazingira.
Aidha, Bw. Elibariki ametoa wito kwa wananchi kushiriki kikamilifu katika upandaji na utunzaji wa miti ili kuhakikisha mazingira yanabaki kuwa salama, yenye afya na endelevu kwa vizazi vya sasa na vijavyo.
Bw. Elibariki ameongeza kuwa upandaji wa miti ni moja ya njia muhimu za kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi, kuboresha ubora wa hewa, kuhifadhi bioanuwai na kuongeza maeneo ya kijani ndani ya Manispaa ya Kinondoni.