31/05/2026
UZALISHAJI WA VIUATILIFU NCHINI KUONGEZA NGUVU, VITA DHIDI YA MALARIA - DKT. SEIF
Na: OWM – TAMISEMI.
Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM- TAMISEMI) anayeshughulikia Afya, Dkt. Jafar Seif amesema hatua ya kampuni ya Tanzania Biotech Products Limited (TBPL) kuwekeza nguvu kwenye uzalishaji mkubwa wa mbolea hai, na viuadudu itakuwa na mchango mkubwa katika kupunguza maradhi ya malaria nchini.
Dkt. Seif ameyasema hayo Mei 30, 2026 Kibaha mkoani Pwani, wakati akizungumza katika hafla ya utiaji saini wa hati ya mauziano ya mbolea kati ya Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) na Tanzania Fertilizer Company (TFC), pamoja na hati za ushirikiano kati ya TBPL, Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI), Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA) na Wakala wa Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA).
Amesema hatua hiyo inaendana na vipaumbele vya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, vya kulinda afya ya jamii na kuongeza thamani ya bidhaa za kilimo, akisisitiza kuwa viuatilifu hivyo vitasaidia kuimarisha mapambano dhidi ya ugonjwa wa malaria nchini.
Kwa upande wake Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Judith Kapinga amesema hatua hiyo itasaidia kuongeza thamani ya rasilimali za ndani, kupunguza utegemezi wa bidhaa kutoka nje ya nchi na kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa.
Aidha, amezitaka halmashauri ambazo bado hazijachukua viuatilifu katika awamu ya tatu kufanya hivyo kwa wakati ili kuwezesha kuanza kwa ugawaji wa viuatilifu katika awamu ya nne, ambapo mpaka kufikia Mei 29, 2026 zaidi ya halmashauri 70 zilikuwa bado hazijachukua vifurushi vya viudadudu vilivyotengwa kwa ajili ya maeneo yao.
Kiwanda hicho kina uwezo wa kuzalisha lita milioni sita za viuatilifu vya kibaolojia kwa mwaka huku kikiwa na masoko ya ndani na nje ya nchi.
30/05/2026
MATIVILA AAGIZA WAKANDARASI KUZINGATIA UBORA KATIKA UTEKELEZAJI WA MIRADI
Naibu Katibu Mkuu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM- TAMISEMI) anayeshughulikia Miundombinu, Mhandisi Rogatus Mativila, amewataka wakandarasi wanaotekeleza miradi mbalimbali chini ya Mradi wa TACTIC kuzingatia viwango vya ubora vilivyoainishwa katika mikataba yao.
Mhandisi Mativila ametoa agizo hilo Mei 29,2026 wakati wa ziara ya ukaguzi wa miradi ya miundombinu inayotekelezwa na TACTIC katika mkoa wa Mara, ambapo amesisitiza kuwa ubora wa kazi ni jambo lisilopaswa kufanyiwa mzaha.
“Katika ziara hii, moja ya mambo muhimu tunayoyaangalia ni ubora wa miradi kwa kuzingatia maelezo yaliyopo kwenye mikataba, hivyo wakandarasi wote mnapaswa kuhakikisha mnatekeleza kazi kwa viwango vilivyokubaliwa,” amesema Mhandisi Mativila.
Ameeleza kuwa wakandarasi wanaposaini mikataba ya utekelezaji wa miradi, wanakuwa wamekubali kutekeleza kazi kwa ubora unaotakiwa, hivyo ni wajibu wao kujisimamia na kuhakikisha wanazingatia masharti yote ya mikataba bila kushurutishwa.
Aidha, Mhandisi Mativila amesema kuwa utekelezaji wa miradi kwa ubora ni sehemu ya kutekeleza maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye amekuwa akisisitiza umuhimu wa kujenga miradi yenye viwango bora ili iweze kudumu kwa muda mrefu na kutoa huduma stahiki kwa wananchi.
Katika ziara hiyo, Mhandisi Mativila amekagua miradi mbalimbali inayotekelezwa chini ya Mradi wa TACTIC, ikiwemo ujenzi wa soko, jengo la Ofisi ya TARURA pamoja na Stendi ya Bweli iliyopo mkoani humo.
30/05/2026
Tupe mrejesho je unarizika na mfumo wetu wa Tausi
29/05/2026
SERIKALI YASISITIZA MIFUMO YA KIDIJITALI KUSOMANA KUONGEZA UFANISI WA HUDUMA
OWM-TAMISEMI
Serikali imewataka Maafisa Tehama katika Sekretarieti za Mikoa nchini kuendelea kuimarisha matumizi ya teknolojia ya habari na mawasiliano ili kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma kwa wananchi pamoja na kuharakisha utekelezaji wa ajenda ya uchumi wa kidijitali nchini.
Wito huo umetolewa na Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Bw. Nicholaus Mkapa, wakati akifunga kikao kazi cha Maafisa Tehama wa mikoa ya Tanzania Bara kilichofanyika Jijini Dodoma, ambapo amesisitiza umuhimu wa mifumo ya serikali kusomana na kubadilishana taarifa kwa usalama ili kuboresha huduma kwa wananchi.
Amesema Serikali imeendelea kusimamia utekelezaji wa ajenda ya uchumi wa kidijitali kupitia uimarishaji wa miundombinu ya umma ya kidijitali (Digital Public Infrastructure), ikiwemo mifumo ya utambuzi wa wananchi, mifumo ya kubadilishana taarifa na huduma za malipo ya kidijitali zinazorahisisha upatikanaji wa huduma mbalimbali.
"Pamoja na mafanikio hayo bado tunao wajibu mkubwa wa kuhakikisha mifumo yetu inaongea, inabadilishana taarifa kwa usalama na huduma zote zinamfikia mwananchi kwa urahisi zaidi," amesema Bw. Mkapa.
Aidha, amewataka Maafisa Tehama kuhakikisha mifumo yote inayotumika katika halmashauri inaunganishwa na mifumo ya kitaifa, huku wakizingatia usalama wa taarifa za wananchi na utekelezaji wa Sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi ya mwaka 2022 pamoja na miongozo yake.
28/05/2026
DKT. SEIF AELEZA MKAKATI WA SERIKALI KUKABILIANA NA UPUNGUFU WA MADARASA
Na: OWM - TAMISEMI
Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu -TAMISEMI, Dkt. Jafari Seif amesema Serikali imeweka mkakati wa kuendelea kutenga fedha kupitia mapato ya ndani ya halmashauri kuhakikisha ujenzi wa madarasa mapya unaambatana na ununuzi wa madawati 15 au seti 40 za viti na meza kwa kila darasa linalojengwa ili kupunguza changamoto ya upungufu wa samani hizo katika shule mbalimbali.
Naibu Waziri Dkt. Seif ameyasema hay o leo Mei 28, 2026 Bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la Mbunge wa Kongwa, Mheshimiwa Isaya Moses Mngulumi, aliyetaka kujua mpango wa Serikali wa kutengeneza na kusambaza madawati katika shule za jimbo hilo Mkoani Dodoma.
Amesema Halmashauri ya Wilaya ya Kongwa ina shule za msingi 133 na sekondari 45, ambapo shule za msingi zina upungufu wa madawati 6,199 sawa na asilimia 23.1, huku shule za sekondari zikiwa na upungufu wa seti 643 za viti na meza sawa na asilimia 3.4.
Kwa mujibu wa Dkt. Seif, katika mwaka wa fedha 2025/26 Halmashauri ya Kongwa imetoa Shilingi Milioni 28.92 kupitia mapato ya ndani kwa ajili ya ununuzi wa madawati 445 na seti 54 za viti na meza, huku mwaka 2026/27 zikitengwa Shilingi Milioni 33.25 kwa ajili ya ununuzi wa madawati 475 na seti 320 za viti na meza.
Aidha, amesema Serikali itaendelea kuhakikisha kuwa ujenzi wa madarasa mapya unaenda sambamba na ununuzi wa madawati 15 au seti 40 za viti na meza kwa kila darasa linalojengwa pamoja na kushirikisha wadau mbalimbali katika kuondoa changamoto ya upungufu wa samani za shule nchini.
27/05/2026
Naungana na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kuwatakia Waislamu na Watanzania wote Sikukuu njema ya Eid al - Adha.