13/05/2026
TANZANIA KUWA MWENYEJI WA MKUTANO WA KIMATAIFA WA WABUNGE WANAWAKE WA UKANDA WA MAZIWA MAKUU
Na Saidi Saidi, WMJJWM – Dodoma
Tanzania inatarajiwa kuwa mwenyeji wa Mkutano wa Kimataifa wa Wabunge Wanawake wa Ukanda wa Maziwa Makuu (ICGLR) unaotarajiwa kufanyika jijini Dar es Salaam kuanzia Novemba 2 hadi 5, 2026.
Hayo yamebainishwa na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Dorothy Gwajima, Mei 13, 2026 jijini Dodoma wakati wa kikao chake na ujumbe wa Jukwaa la Wabunge la Mkutano wa Kimataifa wa Ukanda wa Maziwa Makuu (ICGLR), ukiongozwa na Rais wake Mheshimiwa Sergio Vaz Mbunge wa bunge la Angola , ambapo Waziri Dkt. Gwajima amesema Tanzania imejipanga kikamilifu kuratibu mkutano huo muhimu unaolenga kuimarisha ushiriki wa wanawake katika uongozi, amani na maendeleo endelevu ndani ya ukanda huo.
Aidha, amesema mkutano huo utatoa jukwaa kwa wabunge wanawake kujadili namna ya kuimarisha mchango wa wanawake katika ujenzi wa amani, kuzuia migogoro, kuimarisha utawala bora pamoja na kushiriki katika maamuzi ya kisiasa na kijamii ndani ya Ukanda wa Maziwa Makuu.
Dkt. Gwajima amesisitiza kuwa kuwawezesha wanawake katika nafasi za uongozi ni hatua muhimu katika kufanikisha maendeleo jumuishi na kudumisha amani ya kudumu katika ukanda huo. Pia amesema uenyeji wa mkutano huo unaendana na dhamira ya Tanzania ya kuendeleza ajenda ya Wanawake, Amani na Usalama, hususan baada ya uzinduzi wa Mpango wa Taifa wa Wanawake, Amani na Usalama uliofanyika Agosti 19, 2025.
Kwa upande wake, Rais wa Jukwaa la Wabunge la Mkutano wa Kimataifa wa Ukanda wa Maziwa Makuu (ICGLR) Mhe. Sergio Vaz ameipongeza Tanzania kwa utayari wake wa kuwa mwenyeji wa mkutano huo, akieleza kuwa ushirikiano kati ya Tanzania na ICGLR utaendelea kuimarisha mshik**ano, mazungumzo na maendeleo katika Ukanda wa Maziwa Makuu.
MWISHO
13/05/2026
Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mheshimiwa Dkt. Dorothy Gwajima, amekutana na Sekretarieti ya Jukwaa la Wabunge la Mkutano wa Kimataifa wa Ukanda wa Maziwa Makuu (ICGLR), ikiongozwa na Rais wake Mheshimiwa Sergio Vaz, ambaye ni Mbunge kutoka Bunge la Angola.
Kikao hicho kililenga kujadili kuhusu ushirikiano katika maandalizi ya Mkutano wa Kimataifa wa Wabunge Wanawake wa Ukanda wa Maziwa Makuu (ICGLR) unaotarajiwa kufanyika jijini Dar Es Salaam kuanzia Novemba 2 hadi 5, 2026.
Mkutano huo unalenga kuimarisha ushiriki wa wanawake katika uongozi, amani na maendeleo endelevu ndani ya Ukanda wa Maziwa Makuu kupitia ushirikiano wa kikanda na kimataifa.
13/05/2026
AFRIKA YAHIMIZWA KUJENGA MUSTAKABALI SALAMA KWA WATOTO.
Na Mwandishi Wetu WMJWM Nairobi- Kenya
Mke wa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Neema Mwigulu Nchemba, ametoa wito kwa viongozi na wadau wa Afrika kuweka kipaumbele katika ulinzi wa watoto dhidi ya ukatili wa kidijitali.
Akizungumza jijini Nairobi, Kenya Mei 12, 2026, katika Mkutano wa Wenza wa Mawaziri wakuu wa nchi za Afrika, uliofanyika Pembezoni mwa Mkutano wa “Africa-Forward Summit” ukilenga kujenga mazingira salama ya kidijitali kwa watoto wa Afrika katika ulimwengu unaoendeshwa na Akili Unde (AI) Nchemba alisisitiza kuwa mustakabali wa bara la Afrika hautategemea tu vigezo vya kiuchumi, bali uwezo wa watoto kujifunza na kuvumbua katika nafasi ya kidijitali bila hofu ya unyanyasaji.
Katika hotuba yake, alibainisha kuwa ingawa teknolojia ya Akili Bandia (AI) inatoa fursa kubwa katika sekta za elimu, afya, na ujasiriamali, imeleta pia hatari mpya na halisi. Alitaja changamoto k**a vile uonevu mtandaoni, unyanyasaji wa kijinsia unaochochewa na AI, na ulaghai k**a vitisho vinavyovuruga utu na maendeleo ya watoto barani Afrika.
Ameeleza hatua zilizopigwa na Tanzania, ikiwemo kufanya marekebisho ya Sheria ya Mtoto (Sura ya 13) na kuimarisha utekelezaji wa Sheria ya Makosa ya Mtandao ya mwaka 2015. Aidha, alikumbusha Kampeni ya Kitaifa ya Ulinzi wa Watoto Mtandaoni iliyoanzishwa Februari 2024 na kuundwa k**ati maalum ya wadau mbalimbali ili kuhakikisha mazingira salama kwa watoto.
Mkutano huo, uliandaliwa na Kuongozwa na Mke wa Rais wa Jamhuri ya Kenya, Mama Rachel Ruto ambapo ulihitimishwa kwa wito wa dharura wa kuimarisha ushirikiano wa kikanda na sheria madhubuti.
12/05/2026
MDEMU AWATAKA WANAWAKE KUJIKWAMUA KIUCHUMI NA KUDUMISHA MALEZI BORA
Na Saidi Saidi, WMJJWM – Iringa
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Makundi Maalum, Felister Mdemu, amewataka wanawake kushirikiana katika kujikwamua kiuchumi huku wakiendelea kuthamini familia, malezi bora, kuwaheshimu waume zao na kuhakikisha watoto wanapata malezi yenye maadili mema.
Mdemu amesema hayo Mei 11, 2026 mkoani Iringa, wakati wa mafunzo ya mwongozo wa uanzishwaji na uwezeshaji wa majukwaa ya wanawake kiuchumi yaliyofanyika katika Kijiji cha Kipaduka, Kata ya Uhambingeto, wilayani Kilolo. Mafunzo hayo yalihusisha madiwani pamoja na viongozi wa majukwaa ya uwezeshaji wanawake kiuchumi kutoka kata mbalimbali za mkoa huo.
Akizungumzia umuhimu wa majukwaa hayo, Mdemu amesema ni maono ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, yenye lengo la kuwainua wanawake kiuchumi kupitia elimu ya fedha, ujasiriamali, matumizi ya teknolojia pamoja na upatikanaji wa mikopo na masoko.
Aidha, amesisitiza umuhimu wa wanawake kupata taarifa sahihi, kuunganishwa katika vikundi na kushiriki kikamilifu katika majukwaa hayo ili wasiachwe nyuma kutokana na ukosefu wa taarifa au usimamizi hafifu. Pia amewataka madiwani kushirikiana na taasisi za fedha, sekta binafsi pamoja na wataalam ili kuongeza fursa za kiuchumi kwa wanawake katika maeneo yao.
Naye Diwani wa Viti Maalum kutoka Tarafa ya Kilolo, Mheshimiwa Julieth Mkolongo, akizungumza kwa niaba ya madiwani na viongozi wa majukwaa hayo, amesema wako tayari kutekeleza maelekezo yaliyotolewa ili kuhakikisha wanawake wanapata fursa za kiuchumi kwa maendeleo ya jamii na Taifa kwa ujumla.
Kwa upande wao, baadhi ya wanawake walioshiriki mafunzo hayo wamesema elimu waliyoipata itawasaidia kuendesha vikundi vyao kwa ufanisi, kuongeza kipato pamoja na kuimarisha ustawi wa familia zao.
MWISHO
09/05/2026
WAZIRI GWAJIMA AZINDUA MWONGOZO WA USHIRIKI WA WADAU KATIKA MIKUTANO YA KIKANDA KIMAIFA.
Na, WMJJWM- Dodoma
Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dorothy Gwajima amezindua Mwongozo wa Kuratibu Ushiriki wa Wadau wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum katika Mikutano ya Kikanda na Kimataifa wa mwaka 2024 kwa lengo la kuhakikisha ushiriki wa Tanzania katika mikutano hiyo unakuwa na tija kwa taifa. Uzinduzi huo umefanyika tarehe 09 Mei, 2026 jijini Dodoma.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Dkt. Gwajima amesema mwongozo huo umeandaliwa ili kuweka mfumo madhubuti wa usimamizi, uratibu, ufuatiliaji na tathmini ya ushiriki wa Serikali pamoja na wadau mbalimbali katika mikutano ya kikanda na kimataifa inayohusu maendeleo ya jamii, jinsia, wanawake na makundi maalum.
Amesema mwongozo huo utawezesha uratibu wa shughuli zote kabla, wakati na baada ya mikutano hiyo, hatua ambayo itaisaidia Wizara kufahamu aina ya mikutano inayoshirikishwa wadau wake pamoja na tija inayopatikana kwa maendeleo ya nchi.
Dkt. Gwajima ameongeza kuwa mafanikio ya ushiriki wa kimataifa yanategemea maandalizi madhubuti yanayojumuisha uandaaji wa ripoti za nchi, upatikanaji wa rasilimali fedha pamoja na ushirikishwaji wa makundi mbalimbali ya kijamii yakiwemo wanawake, vijana, wanaume, wazee, wajane na viongozi wa serikali.
Naye Mhadhiri kutoka Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM), Dkt. Sirieli Mchembe, akiwasilisha mada kuhusu utekelezaji wa masuala ya usawa wa kijinsia amesema Tanzania inaendelea kutekeleza ajenda hiyo kupitia sera, mipango na mikakati mbalimbali inayotekelezwa na Serikali kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo ili kufikia usawa wa kijinsia ifikapo mwaka 2030 kwa kuzingatia Malengo ya Maendeleo Endelevu.
Kikao hicho kimewakutanisha viongozi kutoka Tanzania Bara na Zanzibar, mashirika yasiyo ya kiserikali, wahandisi wanawake, majaji pamoja na wadau mbalimbali wa maendeleo ya jinsia na wanawake nchini pamoja na Wizara za kisekta kwa lengo la kutathmini mafanikio na changamoto zilizojitokeza katika mkutano wa CSW70 uliofanyika jijini New York mwezi Machi mwaka huu.
MWISHO
09/05/2026
Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima (Mb) ameongoza kikao cha wadau walioshiriki Mkutano wa 70 wa Kamisheni ya Hali ya Wanawake Duniani (CSW70). Kikao hicho kimefanyika tarehe 09 Mei, 2026 Jijini Dodoma.
Katika kikao hicho, Mhe. Waziri Gwajima amezindua rasmi Mwongozo wa Kuratibu Ushiriki wa Wadau wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum katika Mikutano ya Kikanda na Kimataifa 2024, wenye lengo la kuimarisha ushiriki wenye tija, uratibu na uwajibikaji katika mikutano ya kimataifa.