21/03/2024
WITO WATOLEWA KWA WAFANYABIASHARA KUSAJILI BIASHARA ZAO BRELA.
Wito umetolewa kwa wafanyabiashara hapa nchini kusajili biashara zao ili kupata leseni za biashara hizo kwa lengo la kutambulika na Serikali na kupata taarifa sahihi mahali zilipo, kujua mwenendo wa biashara hizo na Serikali kuelekeza fedha zake kwa wafanyabiashara hao wanaotambulika rasmi.
Wito huo umetolewa Machi 20, 2024 na Mkurugenzi wa Miliki Ubunifu kutoka Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) Bi. Loi Mhando wakati wa maonesho ya ujasiliamali kwa wanajumuiya ya Chuo kikuu cha Mzumbe kilichopo Wilaya Mvomero Mkoani Morogoro kuelekea siku yao ya Mzumbe (Mzumbe Day) inayofanyika chuoni hapo kila mwaka.
Bi. Mhando akifafanua zaidi amesema, wafanyabiashara hawana budi kusajili biashara zao na kupata leseni za biashara wanazofanya, lakini pia kuwa na usajili wa alama za biashara na huduma na utoaji wa leseni za biashara na viwanda huku akibainisha kazi mbalimbali zinazofanywa na BRELA kuwa ni pamoja na kusajili makampuni.
“….Sisi tunatoa wito kwa wakazi wa Morogoro na viunga vyake kurasimisha biashara zao pia wafike Chuo kikuu cha Mzumbe watapata huduma zote zinazotolewa na BRELA” amesema Bi. Loi Mhando.
Katika hatua nyingine Bi. Mhando amesema lengo la kuwepo ndani ya siku tatu katika chuo Kikuu cha Mzumbe ni kutoa elimu kwa wanachuo na wahadhiri kuhusu huduma zinazotolewa na BRELA hususan umuhimu wa kurasimisha biashara kwa wafanyabiashara.
Kwa upande wao wanachuo wa chuo hicho cha mzumbe akiwemo Idi Mohamed amesema kuna urahisi wa kuanzisha biashara na kuirasimisha lengo ni kupata rasmi ulinzi wa kisheria na kumsaidia mfanyabiashara kuondokana na changamoto za kibiashara zinazoweza kujitokeza.
Maonesho hayo ya Ujasiliamali kuelekea Mzumbe Day yana lengo la kuhamasisha kazi za ujasiriamali kwa wanachuo na wahadhiri na yanafanyika kwa siku tatu kuanzia machi 20 hadi 23, 2024.
MWISHO.
19/03/2024
WAJUMBE WA KAMATI YA BUNGE YA MAMBO YA NJE, ULINZI NA USALAMA ‘WAMKUBALIA RC MALIMA’
Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama imekubaliana na Maombi ya Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Adam Kighoma Malima ya kuondoa mifugo ndani ya Pori la Akiba la Kilombero kwa maslahi mapana ya Taifa.
Wajumbe wa Kamati hiyo ya Bunge walifika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa huo Wakiwa katika ziara yao ya kikazi na Mhe. Mkuu wa Mkoa hupo kutoa mapendekezo yake na wao kumhakikishia Mkuu huyo kulitafutia ufumbuzi tatizo la uingizaji wa mifugo katika pori hilo.
Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Vita Rashidi Mfaume Kawawa ambaye pia ni Mbunge wa jimbo la Uchaguzi la Namtumbo, amesema wanajua changamoto hiyo ya mifugo katika bonde hilo na kwamba baadhi ya mifugo hiyo ni kutoka nchi Jirani, hivyo wataenda kulisemea suala hilo Bungeni.
Mambo mengine ambayo Mkuu wa MKoa wa Morogoro aliwaomba Wahe. Wabunge wa Kamati hiyo kuyasemea bungeni ni pamoja na suala la kuthibiti mafuriko ndani ya Mkoa wa Morogoro na kupunguza kasi ya Mmomonyoko wa maadaili ndani ya jamii.
MWISHO
19/03/2024
WAHUDUMU WA MABASI NCHINI KUTAMBULIWA RASMI NA SERIKALI.
Mkuu wa Wilaya ya Morogoro Mhe. Rebeca Nsemwa amesema Serikali Nchini Tanzania kupitia chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) kwa kushirikiana na Mamlaka ya udhibiti usafiri wa ardhini (LATRA) Wameanza kuwatambua rasmi watoa huduma wa mabasi ya masafa marefu na mijini kwa kuwapatia mafunzo yatakayowasaidia kuongeza weledi katika utendaji kazi ndani ya sekta hiyo ya usafirishaji.
Mhe. Rebeca ameyasema hayo Machi 18, 2024 wakati Akifungua mafunzo ya siku tano katika ukumbi wa mikutano za Ofisi ya TAFORI zilizopo Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro.
Mkuu huyo wa Wilaya amesema kupitia Wizara ya Uchukuzi na Wizara Elimu Sayansi na Teknolojia waliwezesha kuwepo kwa mradi huu wa (East Afrika Skills for Transportation and Regional Intergration Project) ambapo unafadhiliwa na Benki ya Dunia (World Bank) kuhakikisha utoaji wa elimu unawafikia watoa huduma ya mabasi na kuwafanya kutambulika na Serikali.
“…Ndugu zangu nimefurahi sana kwa kujali kada hii ya uhudumu wa mabasi ya masafa marefu na mjini kwa kurasimisha kada hii kuwa kada inayotambulika na Serikali….” Amesema Rebeca Nsemwa.
Pia Mhe. Rebeca amekipongeza Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) na Malaka ya Udhibiti Usafiri wa Ardhini(LATRA) kwa kufikia hatua ya kutoa mafunzo kwa Wahudumu wa mabasi ambapo itawasaidia kutoa huduma bora kwa kuzingatia sheria na tarabutu zote za utoaji huduma.
Katika hatua nyingine Mkuu huyo wa Wilaya Mhe. Rebeca Nsemwa ametoa wito kwa viongozi wa chuo kuwa wabunifu na kufanya kazi kwa weledi ili kukifanya chuo cha Taifa cha Usafirishaji kuwa mahala sahihi pakupatia mafunzo mbalimbali.
18/03/2024
WAZIRI MAKAME AMSHUKURU RAIS UJENZI WA SGR, MALIMA AWATAKA WAAKAZI WA MOROGORO KUTUMIA FURSA HIYO.
Waziri wa Uchukuzi Prof. Makame Mnyaa Mbarawa amemshukuru Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutoa fedha za Ujenzi wa Reli ya kisasa ya Mwendo kasi – SGR ambayo inatarajia kuanza safari zake Mwezi Julai mwaka huu.
Prof. Mbarawa amesema hayo akiwa Mkoani Morogoro leo Machi 18, 2024 wakati wa majaribio ya awamu ya pili ya Reli hiyo ya mwendo kasi kutoka Dar es Salaam kuja Morogoro na kurudi Dar es Salaam ikiwa na mabehewa 14.
Amesema, Reli hiyo ni matunda ya Mhe. Samia Suluhu Hassan ambaye anafanya kila jitihada ya kupata fedha za ujenzi wa miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo Reli ya Mwendo kasi ambayo ameagiza ianze kufanya kazi ifikapo mwezi Julai mwaka huu.“yote haya yamekuja kwa sababu ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amefanya kazi kubwa na leo tunaona matunda yake” amesema Prof. Makame Mbarawa.
Kwa upande wake Mkuu wa MKoa wa Morogoro Mhe. Adam Kighoma Malima amesema kituo cha Kilosa cha reli hiyo ya mwendo kasi kitakuwa kiungo kikubwa kwa Uchumi wa Utalii ambapo amebainisha kuwa watalii wengi wanaokwenda Mbuga ya Wanyama ya Mikumi na Hifadhi ya Milima ya Udzungwa watakuwa wanashukia katika kituo hicho cha Kilosa.
Katika hatua nyingine, Mkuu huyo wa Mkoa amewataka wakazi wa Mkoa huo na watanzania wote kwa jumla kuchangamkia fursa hiyo ya kutumia Reli ya mwendo kasi ambayo itasaidia kuwafikisha salama na haraka kutoka Morogoro Kwenda Dar es Salaam na maeneo mengine wanayotaka Kwenda.
Hata hivyo Mkuu wa Mkoa wa Morogoro amewataka Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Mkoa wa Morogoro kuangalia uwezekano wa kujenga miundo mbinu iliyo bora ya Barabara ya kuzunguka kituo cha Reli ya mwendo kasi cha Mjini Morogoro ili miundombinu hiyo ifanane na uwekezaji mkubwa alioufanywa na Mhe. Rais kwa kujenga kituo hicho Pamoja na eneo la kuhifadhia mizigo (Contener Terminar).
13/03/2024
TANROADS, TARURA ZAPONGEZWA UBORESHAJI MIUNDOMBINU.
Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Adam Kighoma Malima amezipongeza Wakala ya Barabara Tanzania - TANROADS na Wakala wa Barabara za Mijini na Vijijini - TARURA Mkoani humo kwa jitihada za kurejesha miundombinu ya barabara pamoja na madaraja ambayo yaliharibiwa na mvua zilizonyesha kuanzia mwezi Disemba 2023.
Mhe. Malima ametoa pongezi hizo Machi 12, 2024 wakati akifungua kikao cha 41 cha Bodi ya Barabara Mkoa wa Morogoro ambacho kimefanyika katika ukumbi wa Magadu uliopo halmashauri ya Manispaa ya Morogoro.
Mkuu huyo wa Mkoa amesema Mvua kubwa zilizonyesha kuanzia mwezi Disemba Mkoani humo zilisababisha uharibifu wa mali na miundombinu mbalimbali ikiwemo barabara na madaraja huku akibainisha kuwa TANROADS na TARURA kwa kushirikiana na taasisi nyingine zilifanya jitihada za kurejesha miundombinu hiyo kwa wakati.
"...nichukue nafasi hii kuwapongeza wataalam wetu wa TANROADS na TARURA na wengine ambao mlishiriki kupambana na kurejesha miundombinu ya barabara, ninawashukuru sana..." amesema Mkuu wa Mkoa.
Aidha, Mhe. Malima amebainisha kuwa Serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hassan imetoa fedha nyingi kwenye utekelezaji wa miradi ya barabara kwa kipindi cha miaka mitatu kuanzia 2021/2022 akitolea mfano bajeti ya TANROADS kwa mwaka wa fedha 2022/2023 bajeti ya matengenezo ya barabara ilikuwa shilingi Bil. 24 na kwa mwaka 2023/2024 ni shilingi Bi. 20.7.
Kwa upande wa TARURA amesema kwa mwaka wa fedha 2022/2023 taasisi hiyo iliidhinishiwa kiasi cha shilingi Bil.26.96 kwa ajili ya matengenezo na miradi ya maendeleo ya barabara na kwa 2023/2024 ilitengewa shilingi Bil. 26.58.
Sambamba na hilo Mhe. Malima ametoa wito kwa wananchi Mkoani humo kulinda na kuhifadhi miundombinu ya barabara na kuwataka viongozi katika maeneo yao kuwachukulia hatua wale wote watakaobainika kujihusisha na uharibifu wa miundombinu ya barabara.
12/03/2024
Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Adam Kighoma Malima amezipongeza Wakala ya Barabara Nchini - TANROADS na Wakala wa Barabara za Mijini na Vijijini - TARURA Mkoani Morogoro kwa kurudisha kwa wakati miundombinu ya barabara na madaraja ambayo yaliharibiwa na mvua zilizonyesha mwanzoni mwa mwaka huu.
Mhe. Malima ametoa pongezi hizo Machi 12, 2024 wakati akifungua kikao cha 41 cha Bodi ya Barabara Mkoa wa Morogoro ambacho kinaendelea katika ukumbi wa Magadu uliyopo katika Manispaa ya Morogoro.
11/03/2024
Wananchi watakiwa kutunza miundombinu ya barabara
Wananchi wilayani kilosa na Manispaa ya Morogoro Mkoani humo, wametakiwa kutunza miundombinu ya barabara inayojengwa na Serikali ikiwa ni pamoja na vyuma vya madaraja ili miundombinu hiyo iweze kudumu kwa muda mrefu kwa faida yao na vizazi vijavyo.
Wito huo umetolewa Machi 10, 2024 na Katibu Tawala wa Mkoa wa Morogoro Dkt. M***a Ali M***a wakati wa ziara ya Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa huo ya kutembelea Miradi ya maendeleo ya sekta ya miundombinu hususan barabara zinazojengwa katika Wilaya hizo.
Dkt. M***a Ali M***a ambaye amemwakilisha mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa huo ambaye pia ni Mkuu wa Mkoa huo Mhe. Adam Kighoma Malima amesema, serikali inatoa fedha nyingi kwa ajili ya maendeleo lakini kuna watu wachache ambao wanarudisha nyuma azma ya Serikali ya kuwaletea wananchi maendeleo na kuwataka kwa umoja wao kuwa walinzi wa miundombinu hiyo.
Akiwa katika daraja la Berega Wilayani Kilosa Dkt. M***a amewataka wananchi wanaoishi Berega na vijiji jirani na daraja hilo ambalo linaunganisha mikoa miwili ya Morogoro na Tanga kuungana na kupanda miti pembszoni mwa mto wa daraja hilo kwa ajili ya kuimarisha daraja hilo ikiwa ni pamoja na kupanda mikarafuu ambayo pia ni faida kwao.
Katika ziara hiyo, Wajumbe wa kamati hiyo wakiongozwa na Katibu Tawala huyo walitembelea miradi ya barabara ya Mfungua kinywa na Kichangani Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro, daraja la mto Berega, Daraja la Mazinyungu Ilonga barabara ya Rudewa - Kilosa na daraja la Ruaha Mkuu na daraja la Ruhembe barabara ya Mikumi - Ifakara Wilayani Kilosa.
Wajumbe hao wa Kamati ya Ulinzi na Usalama wanaendelea na ziara yao katika Wilaya ya Kilombero kwa lengo la kutembelea barabara ya Kibaoni Ifakara, ujenzi wa daraja la Chiwachiwa na ujenzi wa barabara ya Ifakara Mbingu.
MWISHO
08/03/2024
WANAWAKE MOROGORO WANA MCHANGO KATIKA MAENDELEO.
Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Adam Kighoma Malima amesema miongoni mwa makundi yanayochangia ukuaji wa Uchumi wa Mkoa huo ni kundi la wanawake, hii ni kutokana na kundi hilo kuwa na ushiriki mkubwa katika shughuli za kimaendeleo ya kiuchumi na kijamii.
Mhe. Malima amesema hayo Machi 8, 2024 kwenye kilele cha maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani ambapo kimkoa maadhimisho hayo yamefanyika katika viwanja vya shule ya Msingi K/ Ndege iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro.
Mkuu huyo wa Mkoa amewapongeza Wanawake wa Mkoa huo kwa jitihada za kuendeleza maendeleo ya Mkoa huo na kubainisha kuwa Mkoa unasongambele kwa kasi pia amesema Mkoa una malengo mbalimbali ya kimaendeleo ambapo wananwake hao ndiyo msingi wa kuyafikia malengo hayo.
“...niwapongeze akina mama wote wa Morogoro kwa kazi na jitihada mnazofanya katika kuleta maendeleo ya Mkoa wetu...akina mama ni msingi wa mafanikio ya Mkoa wetu wa Morogoro...” amesema Mhe. Adam Malima.
Aidha, Mhe. Malima amesema Taifa lisiloheshimu mchango na nafasi ya wanawake katika shughuli za maendeleo basi Taifa hilo litakuwa limedumaa huku akieleza kuwa uwekezaji kwa wanawake unaibadilisha jamii moja kwa moja.
Katika hatua nyingine, Mkuu huyo wa Mkoa ametumia maadhimisho hayo kuwataka wananchi wa Mkoa huo kuachana na vitendo vya ukatili wa kijinsia ikiwemo ubakaji na ulawiti huku akiweka bayana kuwa Mkoa umejipanga kwa dhati kukomesha vitendo hivyo.
Sambamba na hilo amezitaka taasisi zinazohusika na utoaji wa haki kuendelea kutoa elimu juu ya haki za wanawake hususan walio katika mifumo ya ukatili wa kijinsia.
Naye Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro Bi. Susan Kihawa amesema Mahakama ya Tanzania imefanya maboresho mbalimbali kwenye sheria na haki za wanawake huku akisema kuwa ukombozi wa kifikra na Elimu madhubuti ni jambo linalotakiwa kutiliwa mkazo ili wanawake waweze kutambua haki zao.
07/03/2024
Kitendo cha watu wa jinsia moja kufanya mapenzi na watu kufanya mapenzi kinyume cha maumbile sio utamaduni wa Afrika na ni jambo la hovyo. Kwa sababu hiyo halikubaliki kamwe na linatakiwa kupigwa vita suala hilo na kukomeshwa.
Hayo yamesemwa leo Machi 7, 2024 na Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Adam KighomaMalima wakati wa kikao cha RCC kinachofanyika ukumbi wa Magadu, Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro.